Thursday, June 30, 2005

Kiswahili lugha yetu

Kuna makala mbili za Padre Karugendo zilizopo kwenye blogu ya Ndesanjo kuhusu Kiswahili. Moja ya jambo aliloonya ni kwamba kama Tanzania italala na kufikiri kwamba ni bingwa wa kiswahili, basi kuna siku utasikia wakenya, waganda, wakongo waafrika ya kusini wakiwa ndio waalimu wakubwa wa kiswahili na wakawa wanatengeneza fedha kupitia lugha ambayo Tanzania inaweza kabisa kujisifu ndio gwiji wake. Mambo kama haya yameshatokea duniani si mageni. Wareno katika historia walikuwa wa mwanzo kabisa kufanya tafiti na kugundua mambo mengi lakini wakalala wakaanza kunywa mvinyo wakapitwa na nchi nyingine za ulaya. Sasa hivi Ureno ni kati ya nchi masikini barani ulaya. Mfano mwingine ni wa Malasia na Ghana katika kilimo cha Mawese, nchi hizi mbili zote zilipata uhuru mwaka 1957, Ghana ilikuwa mzalishaji mkuu wa mawese ambayo ni malighafi muhimu sana, Wamalei walikuwa wanakwenda Ghana kujifunza kilimo hicho, waghana walikuwa wakienda Malasia kuwafundisha namna ya uzalishaji wa zao hilo. Angalia leo tofauti iliyopo kati ya Malasia na Ghana. Malasia sasa hivi ni mzalishaji mkuu wa Mawese duniani, wakitumia taaluma ya kisasa. Ghana sasa wanajifunza toka Malasia. Mifano ni mingi. Tunajifunza?

Tuna matatizo gani?

Je unajua kwamba shirika la ndege la Afrika ya Kusini SAA ambalo lilichukua ATC linamilikiwa na Serikali? Mbona wao wanaweza mpaka wananunua mali za shirika la serikali nyingine? Yaani tunatoa mali yetu inayomilikiwa na serikali yetu kwa serikali ya nchi nyingine. Hamu sina.

Mambo ya UKIMWI yapamba moto

Jamani haya mambo ya UKIMWI yanakuwa sasa ni siasa. Kama mtakumbuka siku za nyuma niliandika jinsi Daktari anayetangaza matumizi ya vitamini kama njia ya kusaidi kupunguza madhara ya UKIMWI anavyobanwa. Nimeandika pia kwenya makala yangu ndefu iliyopo ndani ya blogu sasa. Basi siku za Karibuni Waziri wa Afya wa Afrika ya Kusini, Manto Tshabalala- Msimang alionana na huyo Dr. Rath (bingwa wa vitamini) na anaelekea anakubaliana na hoja kwamba vitamini kiasi fulani zina manufaa katika kumsaidia mhathirika. Baada ya hapo akatoa tamko kwamba wananchi wawe na uchaguzi wa dawa zilizopo, wale wanaoweza kupata ARVs waendelee nazo wale wa vitamini na dawa asilia waachwe wachague kwa sababu asilimia 80% ya wagonjwa wanaofika hospitali za serikali huwa wanatembelea waganga wa asili kwanza. Wabunge wa chama cha wazungu cha DA wamekuja juu, sasa wanataka kumshitaki katika baraza la maadili la watoa huduma za afya kwa kuwaambia wanachi wanaweza kuchagua dawa ambazo hazijathibitishwa kutibu kitaalam. Kuna mvutano usio wa kawaida kati ya watetea kampuni za dawa za magharibi na watetezi wa dawa asilia na vitamini. Huu ukasuku wa waafrika kufikiri kila kitu lazima kipitishwe na wazungu utatumaliza. Huyu Waziri ni ngangari sana na si mhumini mzuri sana wa nadharia za UKIMWI zilizoenezwa na nchi za magharibi ambazo kwanza hazina uthibitisho wa kitaalam. Rais Thabo Mbeki pia alikuwa mmoja wa watu waliokuwa wakihoji nadharia ya HIV-UKIMWI. Ukienda kwenye tovuti hii utakumbana na picha yake pamoja na mambo mengi yahusuyo UKIMWI

Tuesday, June 28, 2005

Makala mbili mpya

Nimeandika makala mbili mpya. Moja kuhusu Shirikisho la Afrika Mashariki na nyingine kuhusu utata juu ya UKIMWI. Zisome hapa na hapa. Makala nyingine mpya kuhusu misaada ya nje nitaibandika karibuni.

PSRC ibinafishwe

Hili dude linaloitwa PSRC limekuwa likilalamikiwa kweli kweli. Limekuwa likifanya mambo ambayo yanalalamikiwa mara kwa mara kama kuuza mashirika kwa bei poa, harufu za rushwa na mikataba ya ajabu ajabu. Hii tume iliteuliwa kurekebisha mashirika ya umma sasa inabidi nayo irekebishwe. Inaweza kubinafsishwa. Kubinafisha taasisi inayoshughulikia ubinafsishaji kama PSRC ni aina mojawapo ya ubinafsishaji pia. Unatangaza tenda halafu unapata kampuni binafsi itakayofanya ubinafsishaji, serikali inabakia na kazi ile ile ya kuweka kanuni na kusimamia sera na kuhakikisha ubinafsishaji unafanyika kwa manufaa ya wananchi. Hii ni njia mojawapo ya kuirekebisha PSRC.

Mchakato wa kuwapata wagombea urais

Nilidhani hii hoja sasa basi, lakini kuna watu wameniuliza naonaje mchakato mzima wa vyama vyote vya siasa kuwapata wagombea urais. Mimi sina ugomvi na mchakato mzima unaotumika najua hizo ni taratibu ambazo vyama vimejiwekea na kukubalika. Ugomvi wangu ni watu wanaoshiriki katika zoezi zima la kuwateua wagombea. Nina maana wajumbe wa Halmashauri Kuu na Mkutano Mkuu wa vyama. Je wajumbe hawa wanaofanya maamuzi mazito namna hii wana uelewa gani wa mambo. Hivi kwa mfano ni wangapi wana uelewa wa rais anayetakiwa katika kipindi hiki cha mageuzi mazito na ushenzi unaofanywa na mataifa makubwa kwa nchi changa? Ni wajumbe wangapi wanaoelewa hali halisi au ni wafuata mkumbo tuu? Hivi wajumbe hupatikana kwa vigezo gani? Ni ualiwatani wa vijiweni, uimbaji wa kutukuza vyama au kupandisha bendera za vyama kwenye magenge au biashara? Hawa wajumbe wanafanya maamuzi makubwa sana. Wanajadili taarifa za utekelezaji wa kazi za serikali, wanatoa maagizo kwa serikali, wanateua wagombea urais nakadhalika. Hivyo wajumbe hawa wanatakiwa wawe waelewa kweli kweli si ualiwatani. Ni lazima vigezo viwekwe kwa wanaogombea nafasi katika ngazi hizi za halmashauri kuu na mkutano mkuu kwa vyama vyote la sivyo tutaona maajabu.

Mambo ya Yakobo

Sikutaka kuandika chochote kuhusu sakata la Yakobo Zuma, Makamu wa zamani wa Rais wa Afrika ya Kusini kutimuliwa kwa madai ya rushwa, lakini wapi, wachokozi wametaka niseme lolote. Basi ninasema. Miezi mitatu iliyopita nilijikuta nabishana na jamaa wawili toka Zambia. Hawa jamaa nilisafiri nao kwa masaa kama 18 hivi, tuliongea mambo mengi likiwepo sakata la Rushwa lililokuwa likimkabili Yakobo. Jamaa mmoja kati ya hawa anadai ni mzoefu wa mambo ya Afrika ya Kusini akaniambia; unajua sakata la Yakobo na rushwa si la kweli? Ni uzushi mtupu, ni mambo ya siasa tuu. Nikamuuliza kivipi? Akaniambia ni mambo ya ukabila, Yakobo ni Mzulu, na watu wa kabila la Waxhosa ambalo wanatokea pia Mandela na Mbeki hawataki mzulu awe rais kabisa kwa hivyo wameamua kumzushia kashfa ili wamtose kwa kuwa umakamu wa rais ungempa nafasi nzuri ya kuwa rais. Akaendelea, hata wazungu hawataki wazulu kwa sababu wazulu si mchezo, ni watu wa shari na walipiza kisasi. Kwa hivyo Yakobo amekumbana na janga kama hilo. Uzulu umemponza. Nikamuuliza huyu jamaa, sasa kwa nini wamwache au wampe vyeo mpaka umakamu wa rais? Jamaa haishiwi na hoja. Akaniweka chini na kuniambia: unajua walimweka pale kukimaliza chama cha Inkatha Freedom cha Mongusuthu Buthelezi ambacho kilikuwa na nguvu kubwa miongoni mwa wazulu na sasa si unaona Inkatha hoi? Kamaliza kazi na sasa anatoswa.

Kwa kweli kama si mambo ya aibu waliyokumbwa nayo kina Chiluba basi huyu bwana angeniaminisha kwa sababu mimi kuna jambo moja nashindwa na nitashindwa kuelewa mpaka kesho. Hivi kwa nini kiongozi wa ngazi za juu kama rais, makamu wa rais au waziri mkuu wakumbwe na kashfa za kijinga za wizi au Rushwa? Ukiona kiongozi anakumbwa na kashfa kama hii basi ni mjinga. Hawa watu wanatunzwa kwa kodi za wananchi wakiwa madarakani, wakistaafu wanaendelea kutunzwa mpaka wafe. Si wao tuu mpaka na wake zao hata kama unao wawili watakutunzia mpaka wafe. Sasa kwa nini unaiba tena? Mimi narudia tena, binadamu ni kiumbe wa ajabu kuliko kingine chochote.

Sasa haya ya Yakobo tutangoja tuone kama kweli ni safi au ni mla rushwa tuu baada ya yeye mwenyewe kujitetetea mbele ya mahakama. Hata yeye mwenyewe amesema ni mambo ya siasa na si mla rushwa, tuongoje tuone kama tutamweka kwenye kundi la viongozi wajinga wa Afrika au la. Kutakuwa na kasheshe, huko kwao Durban washabiki wake wamekuja juu vibaya sana, kila waziri mkuu wa jimbo la Kwazulu Natal anapotaka kuwahutubia wananchi, washabiki wa Yakobo wanavuruga mkutano. Hawaambiwi chochote wakaelewa.

Imetokea Karibuni

Dunia hii ina vituko nakuambia. Nilipoambiwa habari hii ya kusikitisha na kufurahisha niligundua binadamu wana mambo si kidogo. Ilikuwa hivi: jamaa mmoja mweupe nina maana mzungu, alikuwa akisafiri toka mji mmoja uitwao Gobabis kuelekea Windhoek huko Namibia akifuatana na mbwa wake na mfanyakazi wa kiume. Kwa vile alikuwa na gari aina ya pick-up, aliamua kukaa na mbwa wake mbele na jamaa akakaa nyuma huku akitwangwa na upepo usio na mfano. Kuepuka kuchapwa sana na upepo ilibidi atizame upande gari linakotokea , kwa wale wazoefu wa kusafiri kwenye magari ya wazi wanajua hii ndiyo njia ya kupunguza kuchapwa na upepo. Jamaa akachochea gari lake, kabla ya kufika walipokuwa wakienda wakapata ajali mbaya, yule mzungu akafa palepale, mfanyakazi na mbwa wakapata majeraha madogo sana. Polisi walipofika kusaidia na kupima ajali wakawa wanamuuliza yule mfanyakazi: hebu tuambie ajali ilivyotokea, jamaa nadhani hakuwa na subira wala hakupepesa macho akawaambia polisi muulize huyo- huku akimnyoshea kidole mbwa. Akaendelea: mimi nilikuwa nikiangalia gari linapotokea kwa sababu ya upepo, marehemu na huyu mbwa ndio waliokuwa wakiangalia gari linapoelekea hivyo walijua kilichotokea. Kwa hivyo mbwa anaweza kuwaelezea vizuri zaidi. Nakuambia polisi hawakuwa na na hamu hata kidogo. Naambiwa mbwa pia alikuwa akilalama kumona tajiri yake akiwa amelala usingizi wa moja kwa moja.

Saturday, June 25, 2005

Kodi na mishahara ya Tanzania

Nashauri kila mtu apitie lile jedwali la mapendekezo ya Mramba katika kubadilisha viwango vya kodi ya mapato ya ajira. Kuna mambo mengi sana unayoweza kucheza nayo kwenye lile jedwali. Kwanza utagundua wafanyakazi wa Tanzania wanalipa kodi kubwa si mchezo. Angalia kwa mfano mtu mwenye mshahara wa shilingi 100,000 kwa mwezi, ina maana kwa miezi 12 atapata shilingi 1,200,00. Mtu huyu atalipa asilimia 18.5 ya mshahara huo kwa mwaka kama kodi. Ina maana atalipa kodi ya shilingi 222,000 kwa mwaka. Kodi yake ya mwaka inamlipa mfanyakazi wa kima cha chini kwa miezi inayokaribia mitatu. Hiki ni kiasi kikubwa cha pesa. Nadhani viwango vya kodi zetu kwa ujumla ni vikubwa kweli. Nadhani wafanyabiashara wadogo na wale wa kati wana nafuu kubwa kwa sababu viwango vyao vya kodi kutegemeana na mauzo kwa mwaka ni vidogo kulinganisha na hivi vya wafanyakazi.

Jambo la pili unaloweza kuona ni kwamba wale wafanyakazi wanaolipwa mshahara ambao tofauti yake na kima kinachotozwa kodi cha shilingi 80,000 ni ndogo wataumia sana. Mfano mfanyakazi anayepokea 90,000 akilipa kodi ya asilimia 18.5 atabakiwa na shilingi 73,500 pungufu ya kile cha kima cha chini, anayepokea 100,000 atapata shilingi 81,500 akishalipa asilimia 18.5 tofauti yake na kile kiwango kinachotozwa kodi ni shilingi 1,500 kwa mwezi. Haya mahesabu si mchezo.

Jambo jingine ninalotaka kuzungumzia ni jinsi Serikali inavyopoteza mamilioni kwa kuwalipa wafanyakazi wake mishahara midogo. Kwa hali ya kawaida, waajiri wengine, wawekezaji, mashirika ya kimataifa na kadhalika yanapoajiri yanaangalia mishahara inayolipwa na mwajiri mkubwa. Kwa maana ya Tanzania, Serikali ndiyo mwajiri mkubwa. Sasa kama mwajiri mkubwa analipa kiduchu na wao watalipa mishahara ambayo si mikubwa sana, hapa serikali inakosa mapato ambayo ingeyapata kupitia hawa waajiri wengine kama wangelipa mishahara mikubwa zaidi. Hili ni suala la kisera linalotakiwa maamuzi. Sikatai kwamba mishahara pia hulipwa kutokana na tija. Kinachotakiwa ni Serikali kuangalia hili upya na kufanya mahesabu ambayo yataleta uwiano mzuri na kuongeza pato kupitia kodi zitokanazo na ajira.

Kuna haya majigambo kwamba Serikali imekuwa ikiongeza mishahara kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita kutoka shilingi 17,500 kwa kima cha chini mwaka 1995 hadi shilingi 60,000 mwaka 2004 kwa mwezi. Hapa ukiangalia tofauti utadhani ni kitu kikubwa kweli kweli na mwanasiasa anatamka tarakimu hizi akiwa ameuma meno yake kwa msisitizo. Tuambie hizo 17,500 zilikuwa zinanunua bidhaa na huduma kiasi gani mwaka 1995 na kwa sasa hizo 60,000 zinanunua kiasi gani? Huo ndio ungekuwa unyambulifu wenye akili lakini tarakimu tuu hazina maana. Kwenye uchumi tunachoangalia ni mapato yananunua nini kwa kipindi kati ya sasa na baada ya muda fulani.

Kitabu cha kusoma

Jamani kuna hiki kitabu nilichokisoma mara mbili kinaitwa Secret Terrorists kilichoandikwa na Bill Hughes. Jamaa huyu amendika mengi sana yote yakihusu jinsi ambavyo Kanisa Katoliki kwa muda mrefu limekuwa likihujumu taifa la Marekani na Dunia kwa ujumla. Baadhi ya madai haya ni Pamoja na Njama za kumuua rais Andrew Jackson aliyechaguliwa kuwa rais mwaka 1828 jaribio lililoshindikana; kuuwa kwa rais William Hendry Harrison aliyechaguliwa kuwa rais mwaka 1841 rais Zachary Taylor aliyechaguliwa mwaka 1848, jaribio lingine la kumuua Rais James Buchanan kwa sumu lililoshindikana; kuuwa rais Abraham Lincoln na John F.Kennedy. Chanzo cha mauaji na majaribio haya kwa mujibu wa mwandishi ni kutokana na marais hawa kupingana na matakwa ya wanaojulikana kama Jesuits chini ya Kanisa Katoliki.

Madai mengine ya nguvu ni pamoja na kuzamishwa kwa meli ya TITANIC mwaka 1912 kwa lengo la kuwaua matajiri watatu maarufu duniani wakati huo Benjamin Guggenheim, Isador Strauss na John Jacob Astro walioonekana tishio katika kuzuia kuanzishwa benki kuu ya Marekani inayomilikiwa na matajiri wachache wa Jesuits.

Vita ya kwanza na pili ya Dunia pia anasema ilianzishwa kwa mkono wa kanisa hilo. Hitler na Mussolini inasemekana walikuwa wakiungwa mkono na Kanisa Katoliki. Matokeo mengine yanayozungumziwa kwenye kitabu hicho ni pamoja na maovu yaliyofanywa na Slobodan Milosevic katika kuwamaliza Wakristo wa Madhehebu ya Kiorthodox huko Serbia miaka ya 1990. Mwandishi anadai muuji si Milosevic bali ni Papa na Kanisa Katoliki hata kumshitaki bwana Milosevic ni uonevu tuu.

Jamaa anaendelea kutupasha kwamba matokeo ya Septemba 11 ni mtiririko huo huo hakuna cha Osama wala nini kama hakukuwa na Osama mwaka huo wa 2001 basi angeundwa Osama mwingine ili kulinda maovu ya hao majamaa.

Jamani yote tisa lililoniacha hoi ni hili dai kwamba: Vatican ilianzisha Uislamu kwa lengo la kuwaangamiza wakristo na wayahudi, kulinda wakatoliki na kuiteka Jerusalemu ili waikabidhi kwa Papa. Katika miaka michache ya mwanzo ya uislamu, waislamu walifanya hivyo lakini ilipofikia hatua ya majenerali wa kiislamu kuisalimisha Jerusalemu kwa papa waligundua kwamba walikuwa na uwezo wakakataa kuisalimisha. Hata vita ya ugaidi inayoendelea leo ni moja ya njia za kuwalipiza waislamu kwa kukataa wakati huo kuikabidhi Jerusalemu kwa Papa. Kwa hiyo vita ya mashariki ya kati itaendelea, watakufa watu kwa maelfu hadi hapo mpatanishi atakapotafutwa na mpatanishi huyo atakuwa papa na kwa vile vyombo vya habari vilivyothibiwa vitashawishi ulimwengu kwamba anayeweza kutatua tatizo la mashariki ya kati ni papa pekee, atafanya hivyo na ataiteka Jerusalem. Hapo misheni itakuwa imefanikiwa kwa sababu lengo limekuwa wakati wote huu ni kuitwaa Jerusalemu.

Nimedonoa tuu kijitabu hiki nakushauri ukisome. Kisome kwa makini nahisi kimeandikwa na msabato. Kwa wale wanaowaelewa wasabato haitakuwa ngumu kuelewa kwa nini ninasema hivyo. Binafsi nina maswali lukuki ya kumuuliza huyu mwandisi najaribu kuwasiliana naye ili anijibu maswali yangu. Nitawaeleza maendeleo ya mjadala wangu na huyu bwana. Mwenye habari ya ziada juu ya madai haya yaweke adharani watu wayaone na wayajadili.

Majadiliano ya Doha

Jumapili ya tarehe 12/6/2005, kulikuwa na majadiliano mazuri yaliyoendeshwa na mwandishi maarufu wa BBC Tim Sebastian huko Doha Qatar. Majadiliano yenyewe yalihusu kama Wanawake wa nchi za kiarabu wawe na usawa kamili. Kulikuwa na pande mbili zilizokuwa zikijadili pamoja na wachangiaji wengine wengi, upande mmoja ukiwa na waunga hoja mkono ukiwakilishwa na mwanamama mmoja ambaye ni mbunge wa kwanza mwanamke nchini Jordan na Bwana mwingine ambaye ni mtangazaji toka Kuwait. Wachangiaji wa upande huu walielekea kuifahamu barabara jamii ya kiarabu. Walionyesha jinsi watu wengi wanavyochanganya mila za asili za uhafidhina za kiarabu na Uislamu. Nilichojifunza toka kwao ni kwamba wanawawake wanavyochukuliwa katika nchi nyingi za kiarabu si ndivyo uislamu unavyotaka bali ni mila za kale za kiarabu.

Upande wa wa pili wa hoja uliwakilishwa pia na mwanamama na bwana mwingine ambao wote wamekulia nchi za magharibi. Hawa pamoja na kuonekana kutoilewa vema jamii kutokana na kuishi nje walionya kuhusu nchi za kiarabu kuiga demokrasia ya magharibi kichwa kichwa. Lingine lililojitokeza ni uelewa kuhusu usawa kwa wanawake. Watu wengine bado wanafikiria usawa ni hali ya mwanamke kubadilika na kuwa kama mwanaume. Ukizungumzia usawa wanasema basi wanawake wakiwa sawa na wanaume ule uanawake wao utapotea, wanafikiri usawa ni mwanamke sasa kuwa mwanaume. Kinachozungumziwa ni nafasi. Mwanamke apatiwe nafasi kama anazopatiwa mwanaume na tuone kama hataweza. Ni lazima tujue kuna tofauti za maumbile ambalo ni suala la kibiolojia tusiloweza kushindana nalo. Mjadala uliitimishwa kwa kura waliounga mkono hoja walipata asilimia 86 na waliopinga walipata asilimia 14.

Hoja ya kutoiga kila kitu toka magharibi ilinifurahisha mno kwa sababu hata kwetu sisi weusi na watanzania kipekee ni mabingwa wa kuiga mara nyingi mambo ya hovyo zaidi kuliko ya msingi. Wakati mmoja Ndesanjo aliandika makala ambapo aliuliza kwa nini kwa mfano tusiige mambo mazuri toka kwa wazungu kwa mfano kuheshimu muda na kutunza mazingira kuliko kuiga mambo ya hovyo kabisa? Huko tuendako kwa kasi hii ya kuiga ni lazima ukiwa na watoto wa jinsia yoyote ile utenge pesa za kusuka nywele na kununua hereni kwa wanao.

Monday, June 20, 2005

Jamani nani anatoa mgao wa saluti?

Nilitaka kukaa kimya bila kutoa maoni yangu kuhusu baadhi ya wabunge kutaka wapigiwe saluti. Mimi nauliza ni nani mtoa mgao wa saluti? Ni waziri? ni nani? Kwa nini asiwagawie tuu. Nadhani wabunge wamegundua kitu kwenye saluti. Ni lazima wakishapigiwa saluti wananchi wa majimbo yao watapata hali nzuri ya maisha, ni lazima uzalishaji wa chakula utaongezeka, ni lazima masoko ya bidhaa zao yatapatikana, ni lazima umasikini Tanzania utapungua kwa kasi ya ajabu. Nina mategemeo kwamba wakipewa mgao wa saluti malengo yanayoitwa ya milenia yanaweza yafikiwe kabla ya muda wake tukaweka historia. Sidhani kama mtu anaweza kudai saluti kama haimuongezei mwananchi hali nzuri ya maisha. Naomba mtoa mgao afikirie hili. Baada ya kufikiria kuwapa wabunge, na ili kasi ya maendeleo iongezeke kwa kishindo, basi na atoe mgao kwa madiwani wa kata zote nao wapewe saluti zao hawa wako karibu na wananchi zaidi kuliko wabunge. Baada ya hapo viongozi wa mitaa, vitongoji na vijiji wapewe mgao wao, asisahau balozi wa nyumba kumikumi. Nadhani hawa waote wakipewa mgao wa saluti basi mwaka kesho mwezi kama huu tutakuwa tumefikisha malengo ya milenia.
Ili kasi ya maendeleo iongezeke kwa kasi ya ajabu na Tanzania iwe nchi ya dunia ya kwanza kwa kwa kipindi kifupi, viongozi wote walio karibu na wananchi wakabidhiwe saluti zao. Viongozi wa dini wapewe. Dini zote. Maaskofu wote. Mapadre wote. Baba Paroko wote. Viongozi wote wa vigango. Wachungaji wote. Mashemasi wote na waingilisti wapewe mgao wao. Masheikh wote akianzia mkuu, wa mikoa wa wilaya na maimamu wote wakabidhiwe mgao wao. Viongozi wa mashirika yasiyo ya kiserikali wapewe pia. Nadhani tukiongeza kasi ya mgao ndivyo na kasi ya maendeleo itakavyoongezeka. Tusibanie saluti la sivyo tutabaki kuwa masikini mpaka kiama.

Wednesday, June 08, 2005

Wabunge na Saluti

Kuna wakati nilionya kuhusu kutaka uheshimiwa kwa nguvu zote. Angalia sasa ile hoja ya saluti imerudi. Soma hapa.

Wanablogu wa Tanzania na Habari za Siasa

Nakumbuka siku za nyuma kidogo Msangi alitoa changamoto kujadili mapendekezo ya mwanazuoni mmoja aliyeonyesha wasiwasi wake kwamba wengi wa wanablogu Tanzania ni waandishi wa habari na pia hupendelea kuandika habari za siasa. Hili la la waandishi wengi kuwa pia wanablogu nitalijadili kwa kirefu wakati mwingine. Nitalihusisha na tabia ya kutafuta habari kwa watanzania. Kuhusu siasa ni kweli kwamba wengi hujadili habari za siasa. Kwa mtazamo wangu ni kwamba mfumo wa siasa wa nchi au siasa zilizopo ndizo hutoa picha kamili ya mwenendo mzima wa kila kitu. Kama siasa ni mbovu basi kutakuwa na teknolojia mbovu, kutakuwa na sera mbovu za elimu, elimu itakuwa duni, miundombinu duni. Kama mfumo wa siasa haueleweki hakuna kitakachoeleweka. Sera za uchumi hazitaeleweka. Kwa kifupi hakuna kitakachoeleweka au kufanikiwa kama kuna mfumo mbovu wa siasa. Wakati wa siku za nyuma tulikuwa tunasema ili tuendelee tunahitaji: watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Unaweza kuwa na watu, ardhi lakini ukakosa siasa safi. Kutakuwa hakuna maendeleo. Siasa safi na uongozi bora vinaendana sana kama una siasa mbovu utakuwa na viongozi wabovu. Huu ndio ukweli. Napenda kuamini kwamba wanablogu wengi wa Tanzania wamegundua hili, na wanajua kabisa siasa zilizopo ni mbovu na ndio maana leo utasikia mtu akisema ni lazima tukitaka tuendelee tusitegemee wafadhili, kesho mtu huyo huyo anasema hatuwezi kuendelea bila msaada wa wahisani. Huku ndiko kukosa mwelekeo wa siasa. Nadhani waandishi wanaona umuhimu wa kuwa na siasa safi kwanza halafu mengine yatakuja tuu. Najiandaa kumwandikia yule bwana mawazo yangu kwa kirefu. Mjadala uendelee.

Elimu ya Dini Tanzania

Hivi ule ufundishaji wa dini katika shule za sekondari umebadilishwa? Wakati tukiwa sekondari kulikuwa na utaratibu mbovu unaofundisha ukristo, uislamu, uprotestanti ukatoliki katika shule. Walikuwa wakija Mapadre, Wachungaji, masheik kufundisha dini. Wakija mnatenganishwa. Waislamu darasa lao, waprotestanti la kwao wakatoliki la kwao. Nilichukia mno utaratibu huu kwani ulikuwa haufundishi elimu ya dini bali dini. Matokeo yake mtu anafundishwa dini nyumbani, kanisani na misikitini na shuleni. Shule ingetakiwa itoe elimu ya dini. Tofauti ni kwamba shuleni watu wanatakiwa wafundishwe kufikiri, kuzielewa dini zote kuanzia za asili na za kuja na wasifundishwe na viongozi wa dini wahafidhina bali wafundishwe na watu wenye upeo mkubwa wa theolojia. Hii inawapa wanafunzi uwezo wa kuzielewa dini kwa undani na kuzijadili bila jazba hata baada ya kuhitimu shuleni. Mwenye uhakika kama mfumo huu umebadilishwa naomba aniambie kama bado tupige debe ubadilishwe.

Afrika na Mikakati ya kuisaidia

Kama kuna bara la majaribio basi ni Afrika. Katika kipindi cha miaka mitano tumesikia mambo kibao ya kusaidi umasikini Afrika; Mara HIPC, Mara Millenium Account Fund, Mara tume ya Blair, mara sijuhi Clinton Fund za UKIMWI mara Bush initiative. Huku kuna mikakati kibao kwa upande wa Afrika lakini yote pia inategeme wafadhili. Sijuhi haya majaribio yatazaa matunda. Sasa hivi Blair na Bush wanajadili pia kuhusu madeni na misada Afrika. Inasemekana watafikia makubaliano karibuni kuhusu kusamehewa madeni lakini kwa masharti fulani. Nakuapia kutakuwa hakuna jipya watakalokubaliana hii ni danganya toto tuu. Tutaambiwa madeni yatasamehewa baada ya masharti kibao kutimizwa. Kuna jipya katika hili? Wasichoonge ni kwamba hayo madeni tunayoambiwa yatafutwa yalitumikaje kwa faida ya walengwa wa Afrika. Utakuta asilimia 60 ya fedha zenyewe zilitafunwa na watu wao halafu tumeshalipa kama mara tatu ya tulivyopewa. Nakuambia kama kuna kufa ndiko huku.

Thursday, June 02, 2005

Kimya kingi

Nimekuwa kimya kwa muda mrefu sasa. Nilibanwa sana na bado nimebanwa. Nilikuwa nasubiri kwa hamu matokeo ya kura ya maoni kuhusu katiba ya umoja wa ulaya yaliyofanyika ufaransa na uholanzi. Matokeo yake nadhani mmeyasikia watu wamekataa. Niliandika makala kuhusu jumuiya ya afrika mashariki siku nyingi lakini sikuitundika kwa vile nilikuwa nangojea kura hizi. Nitaitundika baada ya kuweka machache kuhusu matokeo ya kura ya ufaransa na uholanzi.

KITABU CHA WAGENI