Monday, September 26, 2005

Makala za Padre Karugendo tena

Naweka makala nyingine tano katika kona ya Padre Karugendo. Moja inahusu maslahi ya Taifa. Isome hapa. Soma pia hii hapa inayosema sera tofauti lakini lengo ni lile lile. Halafu kuna nyingine mbili zinazohusu utakatifu wa Mwalimu Nyerere. Zisome Hapa na Hapa. Kwa leo ya mwisho inasema Kanisa si upinzani. Unaweza ukaisoma hapa. Nitaweka makala nyingine siku za karibuni.

Sunday, September 25, 2005

Mamilioni wanaishi Kwa umasikini wa kupindukia Marekani

Wamarekani zaidi ya milioni 37 wanaishi kwa umasikini mkubwa. Hii ni kama asilimia kumi ya wamarekani wote na ni kubwa kuliko idadi ya watanzania wote. Soma mwenyewe habari hiyo HAPA

Friday, September 23, 2005

Ya Zimbabwe kutokea Africa ya Kusini

Licha ya staili ya Bob Mugabe kukamata mashamba ya Wazungu na kuyagawa kwa wazalendo kulaaniwa vikali na baadhi ya nchi, Afrika ya Kusini inataka kujifunza mbinu toka kwa Bob. Soma habari hiyo hapa

Thursday, September 22, 2005

Elimu na Kujifunza

Tarehe 25/08/2005 Chuo Kikuu cha Western Cape kiliandaa mhadhara wa kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere. Hili ni tukio la kila mwaka kukumbuka mchango wa Mwalimu katika Elimu. Mwaka huu mzungumzaji alikuwa Dr. Rosa Maria Torres Waziri wa Zamani wa Elimu Nchini Ecuador. Mama huyu alitofautisha kati ya kupata elimu na kujifunza. Baadhi ya mambo aliyosisitiza ni pamoja na: kumaliza mtaala si sawa na kujifunza, kujifunza hakuanzii darasani, kutojua kusoma na kuandika hakumaanishi ujinga, kujifunza si kusoma vitabu tuu, Elimu si kuongeza idadi ya wanafunzi pamoja na mengine mengi. Huu ulikuwa mhadhara mzuri na wa kufurahisha.

Jamani Ujambazi!!

Ujambazi umepamba tena moto. Nasikia polisi wametangaza msako kabambe. Kama kawaida utakuwa wa siku mbili tatu halafu watakaa tena mpaka vitendo vya ujambazi vizidi tena kupindukia. Sijuhi kwa nini hilo zoezi kabambe lisiwe la kudumu. Mwaka ule walivyouawa polisi ndio kampeni kabambe ilipamba moto wakakamatwa majambazi kibao. Baada ya hapo wakakaa tena mpaka sasa ndio mpango kabambe unatangazwa tena. Sijuhi utadumu kwa muda gani tena. Lakini kwa vile mapolisi wamejeruhiwa hivi majuzi tunaweza kushuhudia tena majambazi yakikamatwa na kuadabishwa kwa nguvu ya soda.
Jambo lingine ambalo linahitaji kuangaliwa kwa makini ni huu mfumo wetu wa fedha taslimu kila mara. Hii inatokana na mfumo duni wa kifedha. Kwa mfano mfanyabiashara kukaa na milioni zaidi ya mia moja kwenye duka la fedha za kigeni. Inatia shaka kama kweli ni fedha ambazo zimefanyiwa biashara jana yake. Kama ni hivyo basi ni biashara kabambe kabisa. Kama sivyo basi kuna watu wanakaa na fedha bila kuziweka benki na hilo linatia mashaka kwa sababu aidha mfumo wa benki ni mbaya au wafanyabiashara wanakwepa mambo fulani. "Cash Economy" ni mfumo mbaya na hatari sana. Fedha taslimu zinashawishi sana majambazi. Mfano wa yale yaliyotokea Dodoma nayo ni matokeo ya mfumo wa taslimu. Mtu kuchukua shilingi milioni nane kwenda kufanya manunuzi au kulipa chochote ni hatari. Simlaumu yeyote. tatizo ni mfumo wetu. Kila kitu kinahitaji taslimu. Wakati umefika kuanza kuharakisha mabadiliko ya hali hii la sivyo huu uporaji wa fedha taslimu utaendelea na kukua kwa kasi ya ajabu.

Monday, September 19, 2005

Makala ya Kuruwiji

Naweka makala nyingine ya Padre Karugendo inayoitwa Kuruwiji. Ni makala ya kuvutia mno. Isome hapa. Soma hii nyingine hapa inayoitwa wanawake na uongozi

Filamu Mpya ya Kiswahili kuhusu UKIMWI

Nimepata taarifa kwamba Filamu mpya ya Kiswahili iliyotengenezwa Marekani iitwayo TUSAMEHE kuhusu UKIMWI inatarajia kutoka hivi karibuni. Itatoka rasmi mwezi ujayo huko Washinton D.C. na baadaye itaonekana nchi zote za Afrika Mashariki. Cha kufurahisha zaidi ni kwamba kati ya waliocheza sinema hiyo watu Saba ni wazungumzaji wa Kiswahili -watano toka Tanzania na wawili toka Kenya. Cha muhimu ni kwamba kilichowaunganisha wote hawa ni lugha ya Kiswahili. Kampuni iliyoandaa filamu hii pia imekwishatoa filamu nyingine iitwayo Bongoland ambayo inaendelea kuuzwa sehemu mbalimbali duniani.
Nadhani Filamu hii imekuja katika wakati muafaka kwa sababu mbili kubwa; kwanza tatizo la UKIMWI ambalo linazidi kukua na athari zake kuwa mbaya kila ukicha, na pili matumizi ya lugha tamu ya Kiswahili. Uwe tayari kwa filamu hiyo ambayo nataraji itakuwa nzuri na ya manufaa kwetu. Unaweza kusoma zaidi kuhusu Filamu hiyo HAPA

Friday, September 16, 2005

Makala nyingine za Padre Karugendo

Katika kona ya Padre Karugendo nimeweka makala nyingine Tano. Moja inaitwa kichwa cha Yohana Mbatizaji, nyingine Mvuvi, nyingine mbili zinahusu uchaguzi mkuu na ya mwisho inamhusu mtoto wa Afrika. Pitia uzisome.

Tuesday, September 13, 2005

Makala za Padre Karugendo

Kuanzia sasa nitakuwa naweka makala za Padre Karugendo katika blogu hii. Makala zake nyingine nyingi pia zipo na zitaendelea kuwepo kwenye blogu ya Ndesanjo. Kwa leo anza kusoma hii hapa anoyouliza Saida Kalori anagombea Jimbo gani? Halafu isome hii nyingine kutoka Tanganyika kwenda Tanzania hapa. Nitaweka kona yake kabisa ambayo msomaji anaweza kusoma makala zake wakati wowote.

Vitabu

Kuna vitabu viwili nitamshauri kila mtu avisome. Mimi nimevisoma vyote, na uzuri vinavutia kusoma na si virefu sana. Cha kwanza kinaitwa Pambazuko Gizani; kimeandikwa na Kalumuna Mboneko. Usithubutu kukikosa. Kimeandikwa kama riwaya lakini ukikisoma utajionea mwenyewe ukweli wa mambo yanayoelezewa humo ndani. Kwa maoni yangu ni kitabu cha kusomwa na kila mtu. Cha pili ni Rai ya Jenerali; kimeandikwa na Jenerali Ulimwengu. Huu ni mkusanyiko wa makala zake alizokuwa akiandika kwenye gazeti la Rai kuanzia 1993 hadi 1995. Makala hizi japo ni za miaka ya nyuma bado ni mbichi utadhani zimeandikwa leo. Tafuta ukisome. Hutajuata kukisoma. Bei zake nadhani ni za kawaida. Pambazuko Gizani ni shilingi 3,000 na Rai ya Jenerali ni 5,000.

Watanzania tuna mawazo mazuri!!

Niko kwenye Basi nasafiri toka Moshi kwenda Dar. Tukikaribia Dar mjadala unaanza kuhusu uchaguzi. Ndani ya basi kuna mama mmoja mbaye niligundua baadaye sana kuwa ni diwani wa CCM huko Moshi. Mama anaanza kusomesha vijana umuhimu wa kuipigia kura CCM. Madai yake ni kwamba CCM imewalea hao vijana, pili CCM imeleta amani na tatu kwa hali ilivyo CCM imeshashinda. Vijana wale walikuwa na hasira sana kwa maneno ya yule mama wakipinga madai yake hayo. Sikupenda kuingilia mjadala ule kabisa lakini mwishoni nilishindwa kuvumilia. Sikutaka kujadili madai mawili ya CCM kuleta amani na kuwalea na kuwasomesha watanzania kwa sababu naelewa jinsi tunavyochanganya haya mambo. Mtu unaposomeshwa kwa fedha za umma watu wanafikiri nini sijuhi. Umma ndio umekulipia, ni umma umekusomesha. Serikali ipo pale kama wakala tuu. Kama huu umma haukulipa kodi serikali haitakuwepo na ni wajibu wake kuutumikia umma wote. Ikishindwa kuutumikia kuna njia za kuiondoa hiyo serikali. La CCM kuleta amani nililijadili katika makala yangu ya utamaduni wa amani(makala hii ipo kwenye kona yangu ya makala ndani ya hii blogu.
Nilianza kubisha pale huyu mama aliposema CCM imeshashinda. Mimi kama mchumi nilifikiria jinsi gharama za uchaguzi zilivyo kubwa na jinsi ambavyo umasikini umetapakaa nchini. Watu bado wanakufa kwa kipindupindu Dar es Salaam! Kwa nini sasa tutumie mabilioni kupiga kura wakati mshindi ameshajulikana? Nilimtupia huyo mama swali hili. Kabla hajajibu kuna bwana mwingine akadakia. " Wewe kama si mjumbe wa NEC hukumchagua Kikwete, lakini sisi tunajua Kikwete ndiye rais, upigaji wa kura ni formality tuu". Nikamuliza kwa nini Tanzania tusianze haka kautaratibu kazuri ambapo kila chama kikishamteua mgombea wake tunaangalia tuu wingi wa washabiki wanaompokea na yule atakayepokelewa na watu wengi ndiye awe rais tuokoe mabilioni ya kupiga kura? Jamaa akasema hapana. Ni lazima kupiga kura. " Si unaona hata mataifa makubwa kama Marekani ni lazima wapige kura?"Aliendelea yule bwana. Nikamwambia kwa nini sisi kama watanzania tusibuni utaratibu wetu ambapo mshindi atajulikana tuu kwa kutazama idadi ya wapokeaji baada ya kutangazwa na chama chake? Baada ya hapo nchi nyingine zinaweza kuiga toka kwetu. Isitoshe tuna uzoefu. Tutamuomba tuu Spika aliyemaliza muda wake atusaidie kwa uzoefu wake wa pale bungeni anapouliza: wanaokubali waseme ndiyooooo..... wasiohafiki waseme siyooooo......- Waliofiki wameshinda na kipengele hiki kimepita. Uzoefu huu utakuwa chanzo kizuri cha kutusaidia tuokoe mabilioni ya fedha za uchaguzi na kusaidia angalau uchimbaji wa visima.

Kimya

Jamani nimekuwa kimya kwa muda mrefu sasa. Nilibanwa na shughuli kibao. Nilikwenda pia Nyumbani kuwaona ndugu jamaa na marafiki. Nyumbani sasa ni kampeni mtindo mmoja, watu kujieleza kwa wananchi, mlungula kutembezwa pale inapobidi, kila mgombea kumtoa mwenzake kasoro na mambo mengine ya namna hiyo. Barabara za Dar zimezidi kuwa finyu, magari ni mengi kuliko uwezo wa barabara. Barabara ya Shekilango iliyojengwa miaka michache iliyopita inatisha. Imebomoka yote. Sinza yote sasa inafanana. Zile barabara za vichochoroni hazina tofauti na barabara kuu ya Shekilango. Cha kusikitisha ni kwamba uwezo wa hii barabara ya Shekilango ni kupitisha magari yasiyozidi tani kumi kama sikosei. Wapi? yanapita mpaka ya tani 30. Ukiongezea na ukweli kwamba hakuna mifereji ya kupitisha maji basi mvua inavyonyesha inazoa kila kitu. Barabara hoi.

KITABU CHA WAGENI