Thursday, August 18, 2005

Simba wazidi kuua watu

Kuna hii habari hapa inayoonyesha jinsi ambavyo idadi ya watu wanaouawa na simba imekuwa ikiongezeka Tanzania. Kuna maeneo mengine watu huamini kabisa kwamba hawa si simba wa kawaida. Huwa wanatumwa kula watu fulani fulani. Kwa maeneo kama hayo hawa huitwa simba watu.

Wednesday, August 17, 2005

Taifa Moja Nchi Mbili


Niliposoma takwimu za umiliki mali na mapato kati ya weupe na weusi Afrika ya Kusini nilishindwa kuamini. Katika takwimu hizo mwandishi alisema kwamba, kama ukiigawa Afrika ya Kusini kama nchi mbili tofauti; moja ikiwa ya wazungu ambao ni asilimia 14 na nyingine ikiwa ya weusi asilimia iliyobaki na ukitumia kigezo cha shirika la maendeleo la umoja wa mataifa –UNDP cha maendeleo ya watu (Human Development Index) ambapo nchi hupangwa kuanzia ya juu kabisa mpaka ya mwisho basi sura itakuwa hivi:
Taifa la wazungu asilimia 14 wanaomiliki asilimia 88 ya mali binafsi (Private Property) litashika namba ya 24 likiwa hatua moja chini ya Uhispania
Taifa la weusi ambao zaidi ya nusu wanaishi kwa kipato cha dola moja kwa siku, na asilimia 40 ya watoto wakiwa wamedumaa kwa utapiamlo litashika namba ya 123 likiwa juu ya Congo hatua moja. Hii inaonyesha ni jinsi gani pengo la walio nacho na wasio nacho lilivyo kubwa.
Nilianza kwa kusema sikuamini hizo takwimu kwa sababu ya picha ya mwanzo niliyokuwa nayo ya sehemu za katikati ya miji ambapo kuna barabara nzuri, nyumba nzuri, mahoteli makubwa, magari ya kifahari na vinginevyo. Sasa nimeamini. Nilishiriki katika utafiti wa maeneo mbalimbali ya Cape Town siku za karibuni tukiwa tunatafiti shule za Msingi. Acha utani. Maeneo wanayoishi weusi ndani ya hili jiji zuri yanatisha. Vijumba vingi ni vya mbao na mabati kote. Msongamano wa ajabu. Shule zao utaziona ziko hoi kabisa. Ukilinganisha na hizo za wazungu utazimia. Za wazungu zimesheneza acha utani. Kila kitu kipo darasani. Wanafunzi utaona tofauti zao za kuelewa mambo kabisa. Si kwamba weusi ni wajinga ila mazingira yanawafanya wasiweze kuwa kama wenzao. Tembea uone. Hapa ni mjini bado sijaenda huko vijijini nijionee.
Gazeti moja hapa siku za karibuni limetoa takwimu za kusikitisha. Inasemekana kwamba kwa sasa wanafunzi 3.6 milioni hawana viti vya kukalia na wengine milioni 4.2 hawana madawati yanayofaa kuandikia (hakuna mweupe hapa). Lakini ukiona maisha ya mijini huwezi kuamini kabisa. Kwa mtaji huu si kwamba kuna watu tofauti tuu katika nchi hii, bali pia hizi ni dunia mbili tofauti kabisa.

Ni nini maana ya kustaafu ?

Hili neno kustaafu linanipa shida sana. Nilidhani maana ya kustaafu ni kwamba uwezo wako wa kutoa mchango katika uzalishaji unakuwa umeanza kupungua na ndiyo maana ukifikia umri fulani ni lazima ustaafu. Kwa Tanzania umri wa kustaafu ni miaka 60. Umri huu uliongezwa miaka michache ya nyuma. Kabla ya hapo ilikuwa 55. Na umri huu hauwekwi tuu kwa maana ya kuwekwa kuna vigezo vinatumika na pengine utafiti unafanyika kabisa kutafuta umri muafaka wa kustaafu. Nadhani ukishastaafu sasa unatakiwa kufanya shughuli ambazo haziumizi sana kichwa na mwili wako, shughuli ambazo kwa kweli hazihitaji kukimbia kimbia. Ukimona mtu anastaafu halafu eti anachukua jembe kwenda kufungua shamba ujue huyo hawezi kuzalisha chochote. Utalima wakati wa uzeeni?

Kama ninachofikiria ni sahihi basi inaelekea bungeni ni mahali pa kupumzikia. Ni mahali ambapo hapahitajiki sana kutumia akili nyingi wala nguvu nyingi kwa sababu watu wengi wanaoijiingiza kwenye ubunge ni wazee waliokwishastaafu. Kwa maana nyingine mchango wao sehemu za kazi walipokuwa wakifanyia ulishapungua. Sasa unampeleka bungeni akawakilishe wananchi wa jimbo lake, akatunge sheria, akaishauri serikali nakadhalika. Hivi kutatokea chochote huko bungeni? Mimi nadhani hapa kuna kasoro kubwa mno. Kuna wale watakaosema kwamba busara za wazee zinatakiwa. Ndiyo zinatakiwa lakini si lazima iwe bungeni wana sehemu nyingine wanazoweza kupenyeza hizo busara. Pili nani alisema kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya busara na uzee? Kuna kuchanganya mambo hapa. Kuna tofauti kubwa kati ya busara na kuona mambo kwa miaka mingi. Labda Kiswahili changu ni kibovu nashindwa kuelewa kama kuona mambo kwa miaka mingi ndiyo busara. Kuna vijana wadogo wenye busara kuliko wazee wa miaka 80!. Na kama hujawahi kuwa na busara udogoni mwako huwezi kuwa nayo uzeeni hata utambike.

Mimi nadhani sasa wakati umefika kwamba ukishafikia umri wa kustaafu uache zile kazi nzito na zenye kuhitaji msuli hasa msuli wa akili. Labda tukubaliane kwamba kwenye siasa hakuna kazi za kutumia nguvu na akili nyingi ndio maana ukishastaafu unaweza kujimwaga na kuanza kwenda kukaa kwenye vikao Dodoma huku usingizi ukikuandama bila kutoa mchango wa maana katika miswada inayowasilishwa. Mawaziri wazee nao huu uwe mwisho wao. Labda pia iwe uwaziri nao ni kazi ya mteremko isiyohitaji nguvu na matumizi ya akili.

Thursday, August 04, 2005

Uajua hili?

Mnamo mwaka wa 1960, Jamhuri ya Afrika ya Kati ilikuwa na hali nzuri kwa zaidi ya asilimia 50 ikilinganishwa na Taiwan, lakini kufikia mwaka 2000, kibao kilikuwa kimegeuka kabisa kwa Taiwan kuwa tajiri mara 17 ya Jamhuri ya Afrika ya Kati. Tukiweka tarakimu ili ieleweke kirahisi ni kwamba; mwaka 1960 kipato cha wastani kwa mwananchi wa Jamhuri ya Afrika ya Kati kilikuwa Dola za Marekani 2,180 wakati cha Taiwan kilikuwa Dola 1430, mwaka wa 2000 kipato cha kila Mtaiwani kilipanda na kufikia dola 18,700 wakati cha Mwanaafrika ya kati kilishuka na kufikia dola 1,120. Hali si tofauti sana ukilinganisha kwa mfano Malaysia na Ghana ambazo zote zilianza kwa kipato kinacholingana mwaka 1960 na zote zikiwa zinategemea sana kilimo, kadhalika unaweza ukalinganisha Nigeria na Indonesia zote zikiwa wazalishaji wa mafuta. Nitajaribu kuandika kwa lugha rahisi sbabu za maajabu haya. Kwa vyovyote unaweza kwa sasa ukachukulia tuu kwamba Afrika tuna kile ambacho tunatumia kujifariji na kuhalalisha uzembe "bahati mbaya" wakati wenzetu wana kile ambacho huitwa "bahati nzuri." Au tuite mkosi kwa Afrika? Sijuhi. Ngoja nitafute muda nichambue sababu ambazo zimekuwa zikitolewa kwa pengo hili.

Monday, August 01, 2005

Wanablogu wanafanya uandishi wa habari je ni waandishi wa habari?

Soma habari hii hapa uone umuhimu wa wanablogu

Blair na aondoke

Soma habari hii inayosema kwamba Tony Blair hafai tena kuendelea kuwa Waziri Mkuu kufuatia kitendo chake cha kusababisha mji wa London ushambuliwe kwa utitiri wa mabomu na sasa kutaka kunyang'anya wananchi baadhi ya haki zao na kuminya uhuru wao kutokana na sheria mpya za ugaidi.

Tutamkumbuka Daktari Garang

Daktari John Garang, makamu wa rais wa Sudan kwa wiki tatu tuu na kiongozi wa Sudan ya Kusini kwa miaka lukuki emefariki wakati ambapo dunia ilikuwa na matumain makubwa sana kwake hasa baada ya kusaini makubaliano ya amani na serikali ya Khartom. Soma habari hii hapa. Garang, Daktari mchumi aliyewahi kusoma Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam miaka ya nyuma na kupata shahada yake ya udaktari wa falsafa katika chuo hiki hapa alijitolea kupigania haki za wasudani kusini ambao walikuwa wakitengwa na mfumo wa utawala wa Khartom. Kifo chake kitakuwa pigo kubwa kabisa hasa ikitiliwa maanani mkataba wa amani wa hivi karibuni. Alale pema Daktari Garang.

KITABU CHA WAGENI